Saturday, September 27, 2014

COUNTINHO,JERRY TEGETE KUONGOZA KESHO

Mbrazili Coutinho na Jerry Tegete
watakuwa miongoni mwa wachezaji
wa Yanga watakaoanza pambano la
kesho la ligi kuu ya Bara dhidi ya
Prisons, kwenye Uwanja wa Taifa,
kocha Marcio Maximo amesema.
Akizungumza na Nipashe jana,
Maximo alisema anataraji wachezaji
hao wataleta mabadiliko ya kiuchezaji
Yanga na kupata ushindi baada ya
kuanza kwa kufungwa na Mtibwa
Sugar wiki iliyopita.
"Nimefanyia kazi mapungufu
niliyoyaona (katika mchezo wa
kwanza) lakini furaha yangu ni
kurejea kwa washambuliaji Tegete na
Coutinho ambao naamini wataongeza
nguvu na kutuletea ushindi kwenye
mchezo wa Jumapili (kesho),"
alisema Maximo.
Uwepo wa Coutinho, Tegete na
Mbrazili mwingine 'Jaja' kwenye safu
ya ushambuliaji na kucheza kwenye
Uwanja wa Taifa kunampa Maximo
moyo wa kuibuka na ushindi wake wa
kwanza nchini kama kocha wa klabu
ya ligi kuu ya Bara.
Maximo ambaye alikuwa mwalimu wa
Taifa Stars kwa miaka minne tangu
mwaka 2006, amesema beki wa
kushoto Oscar Joshua aliyeumia
kwenye mchezo dhidi ya Mtibwa na
mshambuliaji Hussein Javu
hawatacheza.
Wote wanauguza maumivu ya nyama
za paja.
"Wachezaji wengine wote wapo katika
hali nzuri na naamini wataniletea
ushindi."
Kukosekana kwa Joshua kunatarajiwa
kumfanya Maximo amrudishe Mbuyi
Twite kucheza beki ya kushoto.
Maximo ambaye pamoja na timu yake
wanapewa nafasi kubwa zaidi ya
kutwaa ubingwa wa Bara msimu huu,
alishindwa kuzuia mwendelezo wa
rekodi mbaya dhidi ya Mtibwa kwenye
uwanja wa Jamhuri kwa miaka ya
karibuni timu yake ilipofungwa 2-0.

No comments:

Post a Comment