Wednesday, September 24, 2014

OKWI ADAI KUA YANGA WATATULIA TU

Licha ya kupika mabao yote ya Simba
katika mechi yao ya kwanza ya Ligi
Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL)
msimu huu waliyotoka 2-2 dhidi ya
Coastal Union kwenye Uwanja wa
Taifa, Dar es Salaam juzi,
mshambuliaji Emmanuel Okwi
amesema hakuwa katika kiwango
chake.
Okwi, aliyejiunga na Simba dakika za
mwisho kabla ya kufungwa kwa
dirisha la usajili msimu huu akitoka
Yanga, alisababisha mabao yote ya
Simba juzi licha ya mashabiki wa
Yanga kumzomea mwanzo mwisho
jambo analoamini muda si mrefu
watatulia baada ya kurejea katika
makali yake.
Bao la kwanza la Simba lilipatikana
baada ya Okwi kukwatuliwa nje ya
mstari wa eneo la hatari la Coastal
Union, hivyo adhabu hiyo kuzaa
matunda kupitia kwa mpigaji Shabani
Kisiga kabla ya Mganda huyo tena
kutoa pasi ya mwisho ya bao la pili
kwa mfungaji bora wa VPL msimu
uliopita, Mrundi Amissi Tambwe.
Kisiga alifunga kwa 'frikiki'
iliyomshinda kipa wa Coastal, Shaban
Kado wakati mabao ya mabingwa hao
wa Tanzania Bara 1988 yalifungwa na
mtokea benchi Lutimba Yayo na
mshmbauliaji wa zamani wa Gor
Mahia ya Ligi Kuu ya Kenya, Rama
Salim.
Mara tu baada ya mechi hiyo
iliyochezeshwa na refa Jacob Adongo
kutoka Mara kumalizika, Okwi
aliliambia NIPASHE kuwa bado
hajafikia katika kiwango chake cha
kusakata soka.
“Mara nyingi sipendi kuzungumzia
kiwango changu binafsi kuliko cha
timu, tulicheza vizuri kipindi cha
kwanza na Coastal walicheza vizuri
kipindi cha pili,” alisema Okwi.
“Sijafurahishwa sana na kiwango
nilichoonyesha leo (juzi), nitajitahidi
kuongeza mazoezi ili mechi ijayo
niisaidie timu yangu kupata ushindi,”
alisema zaidi Mganda huyo ambaye
muda wote wa mechi ya juzi alikuwa
akizomewa na mashabiki wa Yanga
waliokuwa wameingia uwanjani
kutazama mechi hiyo.
Alipoulizwa juu ya zomea zomea
inayofanywa na mashabiki wa Yanga
dhidi yake, Okwi alisema: “Sina muda
nao, mimi nimeshakuwa mchezaji
halali wa Simba, mambo yote
kuhusiana na Yanga hayanihusu.
Ninaamini nitakapokuwa katika
kiwango changu, hawatanizomea
tena,” alisema.
Okwi, mchezaji wa zamani wa SC Villa
ya Ligi Kuu ya Uganda na Etoile du
Sahel ya Tunisia, amejiunga na Simba
baada ya uongozi wa Yanga
kuwasilisha nyaraka katika Shirikisho
la Soka Tanzania (TFF) zikionyesha
kuwa mkataba wake wa miaka miwili
na nusu na klabu hiyo ya Jangwani
aliousaini Desemba 13, mwaka jana,
umevunjwa.

No comments:

Post a Comment